SUZA chahitaji mawasiliano yenye tija- Profesa Moh’d
Na Nasima Haji, SUZA
UKUAJI wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) umeelezwa kuwa unalazimisha kuwa na mpango madhubuti wa mawasiliano wa kisasa utakaokiwezesha Chuo hicho kukiunganisha na wadau wa ndani na nje ya nchi.
Akizungumza katika ufunguzi wa kikao cha kupitia sera ya Mawasiliano ya SUZA Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Moh’d Makame Haji, amesema ukubwa wa Chuo na kasi ya maendeleo iliyopo ni vyema kuwa na nyenzo za mawasiliano za kisasa zitakazoleta tija.
‘’Leo chuo kina kampasi tisa, nane zipo Unguja na moja iko Pemba wafanyakazi takriban 700 na wanafunzi 7,200 na wanaendelea kuongezeka, kama hatuna mipago mizuri ya mawasiliano itakuwa shida’’, alisema Profesa.
Alisisitiza kuwa moja katika eneo ambalo Chuo kinapaswa kiimarike ni na kionekane katika ukanda wa kimataifa ni hii sera ya mawasiliano.
‘’Hawatotuona, hawatatujua wala hawatotusikia kama hatujafanya mawasiliano yetu yakawa mazuri’’, alisema.’
Alisisistiza kuwa ana matarajio kuwa sera ya mawasiliano ya Chuo cha SUZA inakuwa bora ili kusaidia Chuo na Taifa kujenga misingi bora inayokwenda na wakati.
Warsha hiyo ya siku moja iliwashirikisha wanahabari wabobezi wa Zanzibar ilifanyika huko Maruhubi hivi karibuni.
mwisho