KONGAMANO LA KITAALUMA LA MAADHIMISHO MIAKA 60 YA MAPINDUZI  MATUKUFU YA ZANZIBAR

Vyuo Vikuu vijikite kuichambua historia isipotoshwe-Prof. Nkenda

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Profesa Adolf Faustine Nkenda amesema vyuo vikuu vina jukumu la kuichambua historia kwa uwazi na kiuzalendo kwa kuzingatia kuwa haipotoshwi.

 

Hayo aliyasema wakati akifungua kongamano la kitaaluma  likiwa ni sehemu ya shamra shamra za maadhimisho ya miaka sitini (60) ya Mapinduzi  Matukufu ya Zanzibar

Profesa  Nkenda alisema historia ni uwanja wa mapambano na inatoa fursa kwa watu kuchora picha mbali mbali.

Aliongeza kuwa Mapinduzi katika nchi yoyote duniani yanafanyika kwa lengo la kubadilisha mfumo na kama zilivyo nchi nyengine, Zanzibar imeitumia dhana hiyo  kuleta usawa wa binadamu.

‘Tuna jukumu la kuiangalia kwa macho meupe, uhakika na ukweli  tusije kusababisha vizazi vijavyo kuwa na tafasiri tafauti’, alisema.

Kongamano hilo linabeba kauli mbiu ‘Tuimarishe Uchumi, Uzalendo na Amani kwa Maendeleo ya Taifa Letu’, lilifanyika kwenye ukumbi wa Dkt. Ali Mohamed Shein uliopo Kampasi ya Tunguu Mkoa  wa Kusini Unguja.

 

Naye Waziri wa   Nchi Ofisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi na Utawala Bora, Mhe. Haroun Ali Suleiman, aliwahimiza  kujifunza historia ya Zanzibar .

‘Muelewe historia ya nchi yenyu kwani skuli haisomeshwi kama inavyostahiki. Someni huu ndo wakati wenu,’ aliwakumbusha.  Akizungumzia kuhusiana na maendeleo ya elimu Zanzibar, Mhe.  Haroun alisema  Chuo Cha Taifa cha SUZA kilianzishwa miaka 22 iliyopita kikiwa na wanafunzi  54 na sasa kina wanafunzi 7000.

Haroun aliongeza kuwa  kabla ya Mapinduzi  kama hujulikani huwezi kupata elimu  na mwenye asili fulani anayeishi mjini ni tafauti na anayeishi shamba, hali ambayo kwa sasa ni tafauti.

Aidha, aliongeza kuwa makongamano kama haya  yafanyike kwenye Wilaya za Unguja na  Pemba  ili nao wapate taaluma hii.

Akichangia mada kuhusiana na harakati za ukombozi Zanzibar na Afrika, Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, Mhe. Steven Wasira alisema Mzee Karume alichukia dhulma na alipenda haki na ukichukia dhulma  unachukua hatua.

Aliongeza kuwa Mzee Karume aliamini katika umoja na hivyo kuungana na viongozi  wengine wa Afrika ili kupigania uhuru kwa pamoja.

‘Mapinduzi haikuwa ajali ilikuwa lazima yafanyike kwa njia ya amani yasingekuwa’, alisema.

‘ Historia huwezi kuibadilisha ukiibadilisha utaandika unavyotaka lakini historia itabaki pale pale’, Mhe. Wasira alisema.

Akimkaribisha   mgeni rasmi, Katibu Mkuu Wizara ya Elimu  na Mafunzo ya Amali (WEMA), Khamis Abdallah,  alisema  miongoni mwa  kazi za Chuo kikuu ni kuchechemua fikra ambapo leo wasomi na wabobesi  wana fursa ya kujadili  historia, maendeleo na mafanikio yaliyopatikana kwa kipindi  cha miaka 60 iliyopita.

Akichangia mada ya wasifu wa Hayati  Mzee  Abeid Amani Karume, Ndg. Ali Shaaban  ambaye ni msomi na mtunzi wa vitabu alisema, Mzee Karume  alijenga misingi imara ya kuwaweka watu pamoja  kwa kuondoa dhana ya kujiona bora hali ambayo inasababisha kuleta mfarakano.

Alifafanua kuwa nchi kadhaa zilikuwa na utawala wa  jadi, kabila ama kundi la kidini lilijiona kuwa ni bora na hivyo kupambana  na kundi jengine. Alitoa mfano ya taifa ya Israel ambapo tangu mwaka 1948  lilipoundwa hadi sasa wanaendeleza mgogoro na kuuwana.

‘Baada ya Mapinduzi  Mzee Karume alifuta dhana ya kujiona kuwa mimi ni bora kwani  ikifikia hapo huishia kuuana’, alisistiza

Mshiriki wa kongamano hilo, ambaye pia ni mwalimu wa somo la historia kampasi ya Tunguu Bi. Ziada  Mussa,  alisema kuwa amejifunza mambo mengi ambayo hakuwahi kuyasikia katika historia ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Aidha, alipendekeza makongamano kama haya kuwa endelevu ili kuepusha kuharibiwa historia lakini pia kuwajenga vijana kizalendo.

Mshiriki mwengine  wa mwaka wa kwanza kutoka Kampasi ya Tunguu huko Nkurumah, Ndg. Samuel  Nathania, alisema hakuwahi kuifahamu historia ya  Mapinduzi ya Zanzibar kwani yeye siyo mzaliwa wa Zanzibar, ila amevutiwa na mada zote zilizowasilishwa.

Aliongeza kuwa ameona faraja pia kongamano kuwashirikisha viongozi waliobobea katika masuala mbali mbali ya kitaaluma.

                                                            

Kongamano hilo ambalo liliongozwa na Mwenyekiti, Balozi Mohammed Hamza, lilipambwa na utenzi wa papo kwa papo uliosomwa na Kassim Yussuf,  lilihudhuriwa na wageni mbali mbali hilo akiwemo, Naibu Katibu mkuu Mstaafu wa Chama cha Mapinduzi, wakuu mbali mbali wa SUZA, wanafunzi na wanataaluma kutoka Chuo cha Alsumeit, Zanzibar University na Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere, chuo cha Sayansi na teknoliojia na Chuo Kikuu Huria na Chuo cha Kiislamu

Wengine ni wawakilishi wa Jumuia za vya siasa Tanzania, ACT, Ada -tadea Chadema, wazaazi, vijana, wanawake,  na  waandishi wa habari.