MAHAFALI   YA 19 SUZA

Dkt. Samia  aongeza kasi kuibua wanawake vinara

 

Na Mwandishi Wetu, SUZA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan,  ametoa wito kwa jamii kuunga mkono jitihada za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuongeza kasi ya ushawishi wa wanawake kujiunga katika fani mbali mbali za masomo.

Akizungumza  katika sherehe za mahafali ya 19 katika ukumbi wa Dkt. Ali Mohammed Shein huko Tunguu, Mkoa  wa Kusini Unguja, Dkt. Samia  alisema hivi sasa wakati umebadilika na kwamba wanawake wamekuwa mstari wa mbele kujitafutia maendeleo yao na jamii.

Katika mahafali hayo wahitimu 2012 walitunukiwa vyeti ambapo miongoni mwao  wahitimu 1229 ni wanawake.

 

‘Asilimia 58 ya wahitimu ni wanawake, haya ni matokeo ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Wakati wetu wanawake kila tukienda juu (elimu ya juu) tunapungua leo imekuwa tafauti’, alisema kwa fahari.

Mazungumzo ya Dkt. Samia yaliafuatia na baada ya wasifu wake uliosomwa mbele ya hadhara ya wageni na viongozi mbali mbali waliokuwepo kwenye mahafali hayo kabla ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kumtunuku  Shahada ya  Uzamivu ya Heshima   ya Utalii na Masoko kutokana na  na mchango mkubwa  alioutoa katika  sekta ya utalii na maendeleo ya taifa.

Akizungumzia mchango wake katika maendeleo ya Zanzibar, Dkt. Samia alisema tunzo aliyopokea ni heshima kwa watanzania wote katika kutekekeleza majukumu yake.

Aliongeza kuwa katika kufanya kazi zake alishirikiana na wengi na aliwaita kubadilishana mawazo kazi zao walizofanya na kubaini kuwa walifanyya mambo mengi makubwa ya kuing’arisha nchi.

’ wakati tunafanya yote haya, hatukuwaza kama  zile zitajulikana na kutunukiwa heshima kubwa’.

Miongoni mwa viongozi waliompaisha ni Rais Mstaafu wa awamu ya 6 Dkt. Amani Abeid Karume, ambaye ndiye alimteua kushika nafasi ya Uwaziri katika masuala ya maendeleo ya wanawake na watoto na baadaye Waziri wa Utalii Biashara  na Uwekezaji.
Aidha, miongoni mwa wahitimu waliofuatilia kwa kina wasifu wake na maelezo yake binafsi, walikiri kuwa wasifu wa  Dkt. Samia na maelezo yake hayachoshi kusikiliza kutokana na kusheheni uwajibikaji wa dhati na kujitolea kufanyakazi kwa moyo wa uzalendo.

‘nilitolewa kichochoroni nikapewa Wizara inayoshughulikia masuala ya wanawake na watoto na baadaye Waziri wa  Utalii, Biashara na Uwekezaji. Heshima hii ni kwa bosi wangu, Dkt Amani Karume, nashukuru kwa malezi uliyonipa na leo napata heshima kubwa’ alishukuru huku akimuangalia Dk. Karume.

Akitoa nasaha zake kwa wahitimu, Dkt. Samia  aliwataka kwenda  kwenye jamii na kuzikabili changamoto zilizoko kwenye jamii   kwa mfumo hasi.

Aidha, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, ameeleza kuridhishwa kwake na kuwepo idadi kubwa ya wahitimu wanawake wengi wanaofanya vizuri katika masomo yao.

‘nachukua fursa hii kukupongezeni tena wahitimu wetu hasa wanawake ambao kwa mara nyengine wametokea  kuwa ndiyo wengi kuliko wanaume, wahitimu wanawake ndio wanaoshika  nafasi nyingi za juu katika masomo mbali mbali.

 

Mapema  Makamo Mkuu wa Chuo cha Taifa SUZA, Profesa Moh’d Makame Haji  alisema Chuo kimeandaa programu mpya ya Ujasiriamali na ubunifu ambapo kati ya wahitimu 18 waliotunukiwa vyeti wahitimu 16 ni wanawake.

Katika hatua nyengine, chuo kimetoa  wanafunzi bora ambao wote ni wanawake kwa kila ngazi kama vile Shahada ya Kwanza aliyetoka katika fani ya mazingira ni Rose R Kibiriti, Stashahada ni Farhia farhan Juma aliyehitimu katika fani ya  kinywa na meno na aliyehitimu katika ngazi ya Cheti na Khadija Paquet  fani ya TEHAMA.

Mwisho