Dk. Karume aridhia kuwa Balozi Kigoda cha Karume

Na  Mwandishi Wetu

Rais Mstaafu wa Awamu ya Sita wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Dk. Amani Abeid Karume, amepokea ombi la kuwa Balozi  wa Kigoda cha Karume kinachotarajiwa kuzinduliwa hivi karibuni.

Ridhaa hiyo ameitoa  huko ofisini kwake Mazizini mjini Unguja mbele ya  Uongozi wa Chuo Kikuu cha Taifa (SUZA) uliofika kuelezea hatua mbali mbali zilizofikia  za kuelekea uzinduzi wa Kigoda hiki.

Dk. Karume aliipongeza  Kamati ya Kigoda kwa kuibua wazo hili wakati muafaka ambapo Chuo kinatimiza miaka 23 tangu kilipoanzishwa.

‘’Muda mzuri sana, SUZA kwa sasa imekua kwa kuanza jambo hili’’, alisisitiza.

Alisema kuna taasisi kama hii imeundwa na umuhimu wake unaonekana inavyoeneza  falsafa  za Mwalimu Nyerere na kwamba inatumika vizuri.

‘’Tumeona umuhimu wa taasisi ile  na kwetu  yapo mengi sana ya historia ya Mzee Karume, unapoizungumza historia ya  Zanzibar lazima Mzee Karume atakuwepo’’, alisisitiza.

Aliongeza kuwa yeye ndiye Rais wa Kwanza wa Zanzibar  atakuwa na mchango mkubwa wa kuimarisha taasisi hii mbali na wanafunzi na wananchi kwa jumla.

‘’Wenye rika yangu ambao Mapinduzi na Muungano  umetukuta tumebaki asilimia sita (6) tu (wamefariki), hapo utaona  mahitaji ya historia yalivyo  makubwa kwa vizazi vilivyopo na vijavyo ’’, alisema.

Aidha, Dk. Karume  alisema yuko tayari yeye na familia yake kuunga mkono jambo hili ili kufikia malengo yanayotarajiwa.

Mapema, Makamo Mkuu wa SUZA, Prof. Moh’d Makame Haji alisema  uzinduzi wa Kigoda cha Karume unatarajiwa kufanyika mapema mwezi wa Juni mwaka huu ambapo   wasomi na viongozi mbali mbali wataalikwa.

 Aliongeza kuwa lengo la kumuenzi  Sheikh Abeid Amani Karume ni kuhifadhi, kuenzi na kuendeleza mawazo  na fikra zake katika kuleta ukombozi  na maendeleo ya Afrika.

‘’Taasisi hii itashughulika na  masuala ya  tafiti, makongamano kama hatua ya kumuenzi kwa ukombozi wa Tanzania na Afrika’’, alifahamisha.