Zanzibar  yajivunia kuongezeka idadi ya wahitimu SUZA                          

Na Mwandishi Wetu, SUZA

Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Zanzibar  (SUZA), Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amesifu jitihada za SUZA zinazochangia kuongezeka idadi ya wahitimu mwaka hadi mwaka katika Chuo hicho.

Akitoa hotuba yake  mbele ya wahitimu, viongozi  na wageni kwenye mahafali ya 19 katika ukumbi wa Dkt. Ali Mohammed Shein huko Tunguu, Mkoa  wa Kusini Unguja Dkt. Mwinyi alisema  anaamini kuwa wahitimu hao wameandaliwa  vyema  ili kuingia kwenye ushindani wa soko la ajira.

Akifafanua ongezeko hilo, Dkt. Mwinyi  alisema katika mahafali haya wahitimu 2,012 wanapewa Shahada mbalimbali ikiwa ni sawa na asilimia tisa (9) ilinganishwa na idadi ya wahitimu 1,913 wa mwaka  uliopita. Aidha, alipongeza jitihada za wanawake kuichangamkia sekta ya elimu ya juu ambapo kati ya wahitimu waliotunukiwa Shahada  wanawake ni 1,229.

‘Napenda niupongeze uongozi wa Chuo, wahadhiri, wafanyakazi na uongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kwa mafanikio ambayo Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar  kinaendelea kuyapata katika  kusukuma mbele maendeleo ya nchi yetu’, alisema.

Katika mahafali hayo, wahitimu  43 walitunukiwa  Shahada za Uzamili, wahitimu 692 walitunukiwa Shahada za kwanza, wahitimu 999 walitunukiwa Stashahada na  wahitimu 367 walitunukiwa  astashahada.

Aidha, Dkt. Mwinyi ambaye pia ni Rais Wa  Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ameelezea kuridhishwa kwake na kuwepo programu mpya ya Ujasiriamali  na Ubunifu (Bachelor of Enterprenuership and Innovation) ambapo wahitimu 18 amewatunuku Shahada zao wakiwemo wanawake 16  sawa na asilimia 89.

‘Nimepata faraja kuona kuwa Chuo  kimeandaa maonesho ya ubunifu na jambo la kuzingatia ni kuhakikisha kuwa wanapatikana watakaoweza kutumia elimu yao kubuni na kuvumbua kutakakosaidia kutatua changamoto za jamii, alisema Dkt. Mwinyi.

Katika mahafali hayo, Dkt. Mwinyi  pia amemtunuku Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Shahada ya Uzamivu ya Heshima ya Usimamizi wa Utalii na Masoko ( Doctor of Philosophy in Tourism  Management and Marketing -Honoris causa) kutokana na  na mchango mkubwa  alioutoa katika  sekta ya utalii na maendeleo ya taifa.

Katika hatua nyengine, Dk Mwinyi aliwatunuku  tunzo maalum za heshima viongozi wengine  waliopanda mbegu za uanzishwaji wa Chuo cha Taifa cha SUZA ikiwa ni sehemu ya kuthamini mchango hao. Viongozi hao ni Rais Mstaafu wa Awamu ya tano wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dkt. Salmin Amour Juma ambaye ndio kinara aliyetoa wazo hilo.

Wengine ni  Mawaziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali katika vipindi tafauti  Mhe. Haroun Ali Suleiman na Balozi Omar Ramadhan Mapuri. Aidha, aliyekuwa Katibu Mkuuwa Wizara hiyo kwa muda mrefu naye pia ana mchango mkubwa wa uratibu hadi wazo hilo likaanza kutekelezeka.

Mapema, akimkaribisha Mkuu wa chuo cha Taifa cha SUZA, Waziri wa Elimu  na Mafunzo ya Amali, Mhe. Leila  Hassan ameelezea mafanikio yanayopatikana katika Chuo hicho kama vile  kuwapatia mafunzo wahadhiri katika ngazi mbalimbali za mafunzo na Serikali kuwalipia  ada za masomo  wafanyakazi  zaidi  100  wa  Chuo hicho.

Aliongeza kuwa  wahadhiri hao wapo  masomoni kwenye ngazi mbali mbali kama vile  Shahada ya uzamivu ( PhD) 47, Shahada ya  Uzamili  37, Shahada ya  kwanza 15 na Astashahada  mwanafunzi mmoja.

Alifafanua kuwa  kupitia  Chuo cha SUZA  imeanzisha  maabara ya ubunifu WASTEX Lab Tunguu pamoja na kununu vifaa vya  maabara vikiwemo kompyuta  na vyengine vya Tehama.

Mapema, Makamo Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Moh’d Makame Haji aliipongeza  jumuia ya Chuo ikijumuisha wanataaluma na wendeshaji  kwa kazi nzuri wanayofanya ya kutoa wataalamu wa fani mbali mbali wanaotarajiwa kuwa mhimili mkubwa katika kuchangia ustawi wan chi.

Mahafali hayo  yalihudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Rais Mstaafu wa Awamu ya sita wa Serikali ya mapinduzi ya Zanzibar, Dkt. Amaan Abeid Karume,  viongozi wa serikali na vyama vya siasa, wajumbe  wa Baraza la Wawakilishi na wabunge   wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, wahadhiri wa Chuo cha SUZA, wahitimu, wazazi na walezi na wageni wengine waalikwa.
mwisho